WAKAZI
wa Kata ya Misalai Tarafa ya Amani Wilayani Muheza, wamependekeza kuwepo
kwa kipengele cha adhabu ya kumwagiwa maji ya baridi na kisha kuchapwa
viboko kwa mbunge atakayesinzia akiwa kwenye kikao bungeni. Wamependekeza pia kwamba adhabu hiyo iambatane na kutoruhusiwa kuhudhuria vikao vitatu mfululizo pamoja na kuzuiwa kugombea tena kipindi kingine mara muda wake utakapomalizika. Walitoa mapendekezo hayo kwa wajumbe wa Tume ya maoni ya marekebisho ya Katiba ilipofika Kijiji cha Misalai kukusanya maoni ya wananchi wa Tarafa ya Amani Wilayani Muheza. Shukrani Said (23) ambaye ni mkulima wa Kijiji cha Ziarai Kata ya Misarai wilayani hapa alisema kutokana na baadhi ya wabunge kuonekana mara kwa mara kupitia runinga inayoonyesha vikao vya Bunge kuonekana wakiwa wamesinzia kuna kila haja ya Katiba mpya kuwekwa vifungu vitakavyowabana wasilale bungeni. “Wabunge hatukuwatuma waende wakalale, matokeo yake zinapitishwa sheria zinazotubana, tuliwachagua waende wakatuwakilishe, kwa hiyo kuwe na kipengele cha adahabu ya viboko,” alisema Shukrani na kusisitiza kuwa adhabu hiyo inavyofanyika ionyeshwe kwenye runinga. Richard Lutangilo wa Kijiji cha Bulwa Wilayani hapa alisema pamoja na adhabu ya viboko, Katiba iongeze kipengele cha kumwagiwa maji kila mbunge atakayesinzia na kama haitoshi asipewe ruhusa ya kuhudhuria vikao vitatu mfululizo na pia asiruhusiwe kuchukua fomu ya kuwania nafasi hiyo mara kipindi chake cha miaka mitano kinapomalizika. “Hili la viboko likiwekwa kwenye Katiba litaleta umakini wa wabunge wetu kwani tunawaona inatuhuzunisha sana sisi wapiga kura tunapowaona wakiwa wamelala fofofo bungeni wakati vikao vikiendelea,” alisema Jackob Zephania. Hadi Mlowe (50) mkazi wa Kijiji cha Mgambo Wilayani hapa alipendekeza umri wa wagombea wa nafasi ya ubunge uanzie miaka 45 kwa kuwa amebaini wabunge vijana ndiyo chanzo cha kukosekana kwa nidhamu ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. “Napendekeza katiba mpya iweke ukomo wa umri wa kuanzia kwa nafasi ya ubunge ili kuondokana na chombo hiki muhimu kukosekana kwa nidhamu tunasikia jinsi wabunge vijana wanavyoropoka linaonekana kama ni Bunge la kihuni,” alisema Mlowe. Cleopas Mutabuzi (50) mkulima wa Kijiji cha Misalai alipendekeza madaraka ya Rais yapunguzwe hasa katika kuteua mawaziri, ambapo alitaka waajiriwe na Tume ya Utumishi kwa kufuata taaluma zao na siyo kuchaguliwa kisiasa. Kadhalika nafasi ya Spika, naibu Spika na Katibu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipendekeza zisitokane na wabunge bali waajiriwe kupitia Tume ya Utumishi na baadaye majina yao yapitishwe bungeni kwa ajili ya kupewa baraka na wabunge. Kamati hiyo ya kupokea maoni ya marekebisho ya Katiba ilikuwa wilayani hapa kwa muda wa siku tatu ambapo iliendesha mikutano Majengo, Kwafungo, Mkuzi, Misozwe, Amani na Misalai. |
July 16, 2012
Wabunge wanaosinzia wachapwe viboko
Tweeted this
Like this, be the first of your Friends
Facebook Blogger Plugin by JustNaira.com | Get Widget
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment
Toa maoni yako hapa!