Tweeted this
Like this, be the first of your Friends
MSANII wa filamu Bongo, Elizabeth Michael ‘Lulu’ juzi Jumatatu
aliwaambia ndugu zake kuwa bado anateseka baada ya kesi yake
inayomkabili ya kuhusishwa na kifo cha msanii mwenzake, Steven Kanumba
kupigwa kalenda baada ya suala lake kuhusu umri wake kuamriwa kupelekwa
Mahakama ya Rufaa Tanzania.
Muda mfupi baada ya uamuzi huo
uliofikiwa Mahakama Kuu mbele ya Jaji Twalib Fauz anayesikiliza kesi
hiyo na Lulu kutolewa katika chumba cha mahakama tayari kwa kurudishwa
rumande, msanii huyo aligonganisha macho na mmoja wa ndugu zake huku
akionekana kuchanganyikiwa.
“Bado nateseka,” alisema Lulu bila kuongeza neno lingine hali iliyozua majonzi mazito kwa ndugu yake huyo.
Lulu (pichani) alifikishwa katika Makahama Kuu ya Tanzania ambapo kesi
yake ilitajwa tena mbele ya Jaji Fauz kwa lengo la upande wa utetezi
kuwasilisha vielelezo vya kuthibitisha umri wake ambapo unadai
hajafikisha miaka 18.
UTETEZI WAKWAMA TENA
Hata hivyo, upande wa utetezi ukiwa tayari
kuwasilisha vielelezo vyao, Jaji Fauz alimtaka Wakili wa Serikali,
Elizabeth Kaganda kuzungumza lolote kabla mawakili wa Lulu kutoa
vithibitisho vyao kama ushahidi.
Wakili Kaganda aliibua hoja mpya ya
kupinga vielelezo hivyo kutolewa mahakamani hapo na kusema
wameshapeleka hati ya rufaa kwenye Mahakama ya Rufaa kupinga kujadili
upya umri wa msanii huyo mahakamani hapo.
Awali wakiwa mahakamani
hapo, mawakili wa pande zote walifikia muafaka wa kuujalidi upya umri wa
msanii huyo ambapo serikali ilipeleka vielelezo vya umri wa Lulu kuwa
ni miaka 18.
Hata hivyo, juzi upande huo wa Jamhuri uliomba
kusitishwa kwa zoezi hilo baada ya kukata rufaa ili uendelee kutambulika
kuwa ni miaka 18 aliouandikisha msanii huyo na kutia saini yake
alipokuwa akihojiwa kituo cha polisi baada ya kukamatwa kuhusu kesi
hiyo.
Kufuatia ombi hilo hilo la rufaa, mawakili wa Lulu, Kennedy
Fungamtama, Peter Kibatala na Fulgency Massawe waliushutumu upande wa
Jamhuri kwa kuwasumbua na kuwa vigeugeu kwani wao ndiyo walioomba kesi
hiyo itolewe Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kupelekwa mahakamani
hapo kwa ajili ya kujadili umri.
Jaji Fauz aliipitia nakala ya
barua iliyopelekwa Mahakama ya Rufaa na mawakili wa serikali na kutoa
uamuzi kuwa kesi hiyo ipelekwe Mahakama ya Rufaa kwa ajili ya kutolewa
upya uamuzi wa kujadili umri wa msanii huyo.
DK. CHENI AWATENGANISHA WAZAZI WAKE
Katika hali ya kushangaza, wazazi wa Lulu, hawakukaa pamoja, msanii wa
filamu, Mahsein Awadh ‘Dk. Cheni’ ndiye aliyekaa katikati yao.
Jambo
lililozidisha huzuni mahakamani hapo ni mdogo wake ambaye jina lake
halikupatikana mara moja, kupelekwa kumsamilia sehemu aliyokuwa amekaa
huku akiwa amezungukwa na maaskari magereza.
Hali hiyo ilimfanya Lulu amwage machozi kwa uchungu.
Kesi hiyo itatajwa tena mahakamani hapo Julai 09, mwaka huu kabla ya kuhamishiwa Mahakama ya Rufaa.
Source: Global publishers