StatsCrop - Free website analyzer!

Ads 468x60px

AddToAny

Lorem

Social Icons

June 25, 2012

SAKATA LA MGOMO MADAKTARI: HALI TETE

Tweeted this Like this, be the first of your Friends

Sakata la mgomo uliotangazwa na madaktari katika hospitali zote za serikali nchini huenda makali yake yakaongezeka na kuleta athari kwa wagojwa, baada ya Jumuiya ya Madaktari kusema kuwa huduma zote za dharura zitasitishwa kwenye hospitali zote nchini kuanzia leo.
Mwenyekiti wa jumuiya hiyo, Dk. Stephen Ulimboka, alisema jana kwa njia ya simu kuwa, huduma za dharura zitasitishwa katika hospitali hizo kutokana na serikali kutoonyesha nia ya kutatua madai yao kama ilivyotoa ahadi na badala yake kinachofanyika ni propaganda tu.
Dk. Ulimboka alisema wanashangaa kusikia kuwa serikali imeweka zuio mahakamani kushinikiza madaktari wasigome, hatua ambayo alidai ni propaganda tu zinazofanywa na serikali kwani madaktari hawajapewa rasmi taarifa hizo.


“Kauli za serikali na zuio la mahakama tunazichukulia kama ni propaganda tu, kwanza sababu hilo zuio hatujalipata rasmi zaidi ya kusikia kwenye vyombo vya habari, kwa hali hiyo kesho (leo) wagonjwa watakuwa na wakati mgumu sana, maana tumekusudia kusitisha huduma zote za dharura katika hospitali zote nchini, ” alisema.

Alisema ufumbuzi wa mgogoro wa madaktari na serikali unashindwa kupatikana haraka kwa sababu viongozi wakuu wa serikali wanaelezwa mambo ya uongo na watu wa chini jambo linalopelekea kutokuwa na habari sahihi za utekelezaji wa madai yao.

Alisema kutokana na serikali kupuuza madai yao italazimika kuwajibika kikatiba katika suala la kuwahudumia wagonjwa ambao wataendelea kupata tabu kwa kukosa huduma za matibabu.

HUDUMA za matibabu kwa wagonjwa jana ziliendelea kuzorota katika baadhi ya hospitali, hali iliyotajwa kuwa inatokana na mgomo uliotangazwa na madaktari.Madaktari walitangaza mgomo wa kutotoa matibabu nchi nzima kuanzia juzi, wakishinikiza Serikali kutekeleza madai yao likiwamo la kuboreshewa mishahara na mazingira ya kazi.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili katika Hosptali ya Taifa ya Muhimbili (MNH),Taasisi ya Mifupa (MOI) na hospitali nyingine za Jiji la Dar es Salaam, umebaini kuzorota kwa utoaji huduma.
Katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, uchunguzi ulibaini mbali na ulinzi kuimarishwa, huduma za matibabu kwa wagonjwa zilizorota, na katika baadhi ya wodi wagonjwa walikuwa hawajatembelewa na madaktari tangu Ijumaa.
Mmoja wa watu ambao wanauguza mgonjwa wao katika wodi namba 4 katika Jengo la Mwaisela, Vicky Rehani alisema mgonjwa wao alipelekwa hospitalini Ijumaa na hadi jana, alikuwa hajapata huduma yoyote akiwa wodini.

"Mapokezi kweli alionana na daktari akamuandikia dawa na kulazwa katika wodi hii, lakini cha ajabu hadi sasa hakuna huduma yoyote ambayo ameipata," alisema .
Katika wodi zilizopo katika Jengo la Kibasila baadhi ya wagonjwa walidai kuwa, kuna madaktari ambao wamefika wodini, lakini hawakufanya mzunguko kama ilivyo kawaida, na hawakuwa na wasaidizi wao ambao ni wanafunzi wanaokuwa katika mafunzo kwa vitendo.
Daktari mmoja aliyekutwa katika wodi ya Sewahaji (alikataa kutaja jina lake), alipoulizwa kuhusiana na kuwapo kwa mgomo alikataa kusema lolote kwa madai kuwa si Msemaji wa MNH.
"Siwezi kusema lolote, kwani hata mimi mwenyewe nimefuata matibabu," alisema daktari huyo na kuongeza kuwa kama mwandishi anataka kujua kama kuna mgomo au la, basi aende hospitalini hapo kesho.
Hata hivyo, uchunguzi zaidi hospitalini hapo umebaini kupigwa marufuku kwa mikusanyiko ya aina yoyote na hata bustani inayotumiwa na wagonjwa na jamaa zao ambayo ipo mbele ya Jengo la Mwaisela, ilikuwa chini ya ulinzi.
"Hapa haruhusiwi mtu yeyote kukaa, amri hiyo imetoka tangu jana (juzi)," alisema mlinzi aliyekutwa eneo hilo na kuongeza kwamba hata mikusanyiko ambayo haieleweki imepigwa marufuku ndani ya eneo la hospitali.
Hali hiyo pia iliwakuta baadhi ya waandishi wa habari ambao walifika hospitalini hapo na kujikuta wakizuiwa na walinzi kuingia katika baadhi ya wodi.
Msemaji wa Hospitali hiyo, Aminieli Eligaesha wakati wote simu yake ilipokuwa ilikuwa inaita bila kupokelewa, hali ambayo ilijitokeza pia juzi Jumamosi.
Wakati hali ikiwa hivyo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na Moi, uchunguzi uliofanywa katika Hospitali za Mwananyamala, Amana na Temeke ulibaini kuwa huduma ziliendelea kwa kusuasua huku baadhi ya wahudumu wakisisitiza hatma ya mgomo huo itafahamika leo.
“Ukitaka kujua sura ya mgomo subiri kesho (leo) itadhihirika kama kweli madaktari wamegoma au la, lakini kwa leo huduma zinaendelea kwa kusuasua, bado tunaangalia Serikali itatoa majibu gani,” alisema mmoja wa madaktari katika Hospitali ya Amana, ambaye hakutaka jina lake kutajwa.
Aliongeza kuwa jana haikuwa siku ya kugoma, bali ni kushinikiza Serikali kutekeleza madai yao na kwamba, kama itaendelea na msimamo wake huduma zote zikiwamo za dharura zitasitishwa.
Hata hivyo, huduma katika Hospitali ya Amana jana zilikuwa zikiendelea huku baadhi ya wagonjwa wakisema kasi ya upatikanaji matibabu ni tofauti na kipindi ambacho mgomo ulikuwa haujatangazwa.
Katika Hospitali ya Mwananyamala, hali ya matibabu pia iliendelea kwa kusuasua na ulipotafutwa uongozi wa hospitali hiyo kuzungumuzia hali hiyo juhudi hizo hazikuzaa matanda.
Katika Ofisi ya Utawala, mwandishi alikutana na mmoja wa wafanyakazi ambaye alikataa kutaja jina na kueleza kuwa Mganga Mkuu alikuwa amekwenda kutembelea wagonjwa wodini.
“Mimi si msemaji. Hili anaweza kuzungumza Mganga Mkuu, lakini amekwenda kutembelea wagonjwa wodini na ameniambia akimaliza kazi hiyo anakwenda kufanya shughuli ya upasuaji, hatakuwa na muda wa kuzungumza nanyi,” alisema ofisa huyo.
Wakati hali ikiwa hivyo Mwananyamala, katika Hospitali ya Temeke pia huduma ziliendelea kutolewa huku baadhi ya watu waliokwenda kuhudumia wagonjwa wao wakibainisha kuwa kasi imepungua.
Katibu wa Jumuiya ya Madaktari, Edwin Chitage alisisitiza, “Sisi tunaendelea na mgomo kama kawaida, tutafanya hivyo hadi Serikali itakapotekeleza madai yetu, na hadi sasa hatujapata taarifa zozote kutoka serikalini,” alisema Chitage.

KCMC vuguvugu laendelea
 Katika Hospitali ya Rufaa KCMC Moshi, madaktari ambao hawako zamu wamekubaliana kufanya kikao cha dharura kuhakikisha hakuna daktari atakayeingia kazini leo.

Wakizungumza na gazeti hili baadhi ya madaktari ambao hawakupenda majina yao yaandikwe gazetini, walisema wamepanga kufanya kikao cha pamoja ambacho kitaweka mikakati ya jinsi ya kufanya mgomo mkali leo, tofauti na ilivyokuwa juzi na jana.

“Mgomo uko palepale kama unavyoona walioko kazini ni wale wenye zamu, tumewataka wasaini, lakini kesho hakuna atakayeingia kazini na mgomo utakua mkali, tumekuwa wapole sana, lakini Serikali imetupuuzia,” alisema mmoja wa madaktari.

Chama cha Tiba Asilia
Kwa upande wa Chama cha Watabibu wa Dawa za Asili (ATME), kimewataka madaktari kuacha kugoma na badala yake waendeleze mazungumzo na Serikali ili waweze kufikia muafaka.

Chama hicho kupitia Mwenyekiti wake, Abudulhaman Simba, kimesema mgomo wa madaktari unahatarisha uchumi wa taifa na haki za wagonjwa, hasa wale wenye kipato cha chini.

Mkoa wa Mwanza
Mkoani Mwanza madaktari walio kwenye mafunzo na wale walioajiriwa waliendelea na mgomo wao jana.

Mmoja wa madaktari bingwa wa Hospitali ya Rufaa Bugando ambaye hakutaka jina lake litajwe, alisema mgomo huo kwa sasa haujaonyesha athari kubwa kutokana na kuwa siku za mapumziko.

"Leo (jana) na jana (juzi), hapajatokea athari za mgomo, tunadhani athari itakuwa kubwa katika siku za kesho (leo) na kuendelea kwani wakigoma hawa wa mafunzo na hao wengine, kazi inakuwa kubwa kwetu," alisema.

Katika hatua nyingine, mgomo huo haukugusa Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru kwani huduma ziliendelea kama kawaida.

Gazeti hili jana lilishuhudia wagonjwa wakipewa huduma za matibabu pamoja na mgomo uliotangazwa kudai maslahi yao.

Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Dk Omary Chande alisema pamoja na kutangazwa mgomo wa madaktari, Mount Meru haijaathirika na mgomo huo.

Wagonjwa waondolewa Mbeya
Katika Hospitali ya Rufaa Mbeya, mgomo uliendelea na kusababisha baadhi ya wagonjwa kuanza kuondolewa hospitani hapo pia na ile ya wazazi, Meta, kwa ajili ya kwenda kutafuta matibabu kwenye hospitali nyingine za watu binafsi.
Mwananchi jana lilishuhudia baadhi ya wagonjwa wakipandishwa kwenye magari na kuondoka kwenda kutafuta matibabu hospitali za watu binafsi.
Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa Mbeya, Dk Eliuter Samky alipoulizwa alikiri kuwepo kwa mgomo wa madaktari walio kwenye mafunzo ya vitendo wanaofikia 70.
Hata hivyo, Dk Samky alisema anao uhakika kuwa madaktari 10 bingwa waliojariwa na Serikali wataendelea kufanya kazi, na hivyo huduma kwa wagonjwa hasa wale walio katika hali ngumu na wale wa dharura zitaendelea kupatikana.
Ombi la wagonjwa
Wagonjwa jijini Tanga,wameiomba Serikali kutekeleza kwa vitendo ahadi iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete kwa madaktari ili kuondoa misunguano iliyojitokeza.

Ombi hilo walilitoa jana walipokuwa wakizungumza na Mwandishi wa habari hizi katika wodi za majeruhi na watoto katika Hospitali ya Mkoa wa Tanga ya Bombo.

"Tunamuomba Rais atekeleze ahadi yake aliyotoa kwa madaktari, wanapogoma sisi walalahoi ndo tunaokufa na wengine kupata madhara zaidi, lakini wao wanapougua wanakwenda hospitali za nje ya nchi," alisema Adamu Abdurahman aliyelazwa katika wodi ya majeruhi ya
Galanosi.

Madaktari waliokuwa zamu katika wodi za Hospitali hiyo walisema hawaamini kama kweli Serikali haina fedha za kuwalipa, kwani kunapotokea masuala mengine imekuwa ikitoa bila ya matatizo.


HUDUMA MUHIMBILI ZASUASUA

Katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, jana utoaji wa huduma kwa wagonjwa zilikuwa zikisuasua ambapo wagonjwa walieleza hali hiyo ilianza kujitokeza tangu juzi.

Katika wodi ya watoto, wauguzi waliokuwa wanaonekana wakifanya kazi ni wale walioitwa kwa dharura na wengi wa madaktari hawakuonekana katika sehemu zao za kazi.
Mmoja wa daktari katika wodi hiyo, ambaye aliomba jina lake lisiandikwe gazetini alisema, wameamua kusitisha huduma mpaka serikali itakaposikiliza hoja zao za msingi.
Alisema watoto wengi wanakufa kwa ukosefu wa hewa ya oksijeni wanapofanyiwa upasuaji kutokana na kukosekana kwa vifaa vya kuvutia hewa.
Alisema kamati iliyoundwa na Rais Jakaya Kikwete kutatua matatizo yanayowakabili madaktari imekuwa ikidharau vikao hivyo, na kila siku wanapokutana kunakuwa na watu wengine tofauti na wale waliokutana nao awali.

“Kila kikao tunachokaa na wawakilishi kutoka serikalini wanakuwa wapya, kikao hiki wanakuja hawa, kikao kinachofuata wanakuja wengine wapya, jambo linalopelekea kutopiga hatua katika mwafaka,” alisema daktari huyo.
Daktari huyo alisema wanamshangaa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hussein Mwinyi kwa kauli yake ya kusema anataka kuzungumza na madaktari upya wakati anafahamu kuwa mazungumzo na serikali yameshafanyika mara kadhaa bila ya kuafikiana madai yao.


HOSPITALI YA TEMEKE
Msimamizi Mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Rolesta Kinunda, alisema hakuna mgomo kwa madaktari wanaendelea na kazi kama kawaida na wanaendelea kupokea wagonjwa kutoka maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam.
Huduma katika hospitali hiyo zilionekana kuendelea kama kawaida, ambapo madaktari walionekana wakipita wodini na kutoa huduma kama kawaida.
Rashid Ndwangila, mkazi wa Mbagala, ambaye amelazwa kwenye wodi namba saba ya wanaume hospitalini hapo baada ya kufanyiwa operesheni ya henia alisema kwa jana madaktari walipita kama kawaida na kuwahudumia wagonjwa wote kwa kuwapatia dawa pamoja na kuwafunga vidonda.


AMANA NA MWANANYAMALA
Huduma katika hospitali hizo zilionekana kuendelea kama kawaida ambapo wagonjwa walikuwa wakihudumiwa na madaktari.


MBEYA: JAMAA WAONDOA WAGONJWA 
Baadhi ya jamaa wa wagonjwa wameanza kuwaondoa katika Hospitali ya Rufaa Mbeya kwa ajili ya kwenda kutafuta matibabu kwenye hospitali za watu binafsi.


NIPASHE jana liliwashuhudia baadhi ya wagonjwa wakipandishwa kwenye magari na kuondoka kwenda kusikojulikana.


Averine Ngeya, mzazi wa mtoto Miliam Alex ambaye ameungua vibaya kwa maji ya moto, alisema tangu juzi baada ya madaktari kuanza mgomo, wagonjwa hawapati huduma nzuri za matibabu zaidi ya kupewa na wauguzi vidonge vya kutuliza maumivu.


“Tangu jana (juzi) hakuna matibabu ya maana ambayo mwanangu ameyapata, wauguzi ndio wanatupatia panado za kutuliza maumivu na kutuambia kuwa tusubiri daktari anaweza kuja wakati wowote, lakini madaktari hawatokei,” alisema Ngeya.


Nipashe limetembelea katika Hospitali ya Rufaa ya Wazazi iliyopo eneo la Meta mjini hapa na kushuhudia eneo la hospitali likiwa halina watu kutokana na matangazo yaliyobandikwa kwenye mbao za matangazo na kuta za hospitali hiyo yakionyesha kuwa hakuna huduma.


Ofisi za hospitali hiyo na ile ya rufaa zilikuwa zimefungwa na wauguzi waliokuwa vibarazani walikataa kuzungumza lolote kuhusiana na hali hiyo kwa madai kuwa wao sio wasemaji.


Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa Mbeya, Dk. Eliuter Samky, alithibitisha kuwepo kwa mgomo wa madaktari walio kwenye mafunzo ya vitendo wanaofikia 70.


Hata hivyo, alisema anao uhakika kuwa madaktari 10 bingwa wataendelea kufanya kazi na hivyo huduma kwa wagonjwa hasa wale walio katika hali ngumu na wale wa dharura zitaendelea.


KCMC WAENDELEA KUGOMA


Mgomo huo umeiathiri Hspitali ya Rufaa ya KCMC mjini Moshi, ambapo inasemekana kila idara ina
daktari mmoja wa zamu huku wengi wakiwa kwenye mgomo.


Habari ambazo zimethibitishwa na baadhi ya madaktari waliopo kwenye mgomo zinasema sio rahisi kubaini athari kwa kuwa jana ilikuwa siku ya mapumziko.


“Kuanzia leo (kesho) ndio athari za mgomo wetu zitaonekana vizuri, kwani tutaachia maeneo yote na kubakiza eneo la wagonjwa mahututi na majeruhi wa ajali mbalimbali,” alisema daktari mmoja na kuongeza: “Lengo si kuwaumiza wananchi bali kuishinikiza serikali kutekeleza madai yetu.”


Mwanahamisi Ally aliyelazwa wodi ya majeruhi na Haji Rashidi anayemuhudumia baba yake katika wodi namba mbili, walisema huduma si za kuridhisha sana kwani kuna mabadiliko ya wazi tangu madaktari walivyotangaza mgomo na wanaoumia zaidi ni wagonjwa, madaktari hawaonekani wakitoa huduma na hata wakihitajiwa hawaonekani.

“Tunaiomba serikali kumaliza tatizo hili kwa haraka, sidhani kama mahakama inaweza kuwa ndiyo suluhisho la kushinikiza madaktari warudi kazini, wakirudi kwa mtindo huo hali haitakuwa nzuri,” alisema Rashid.

DODOMA 34 WAGOMA

Madaktari 34 walioko katika mafunzo kwa vitendo katika Hospitali ya Rufani ya Mkoa wa Dodoma, juzi hawakufika kazini licha ya kutakiwa kuwepo.

Hata hivyo, huduma  katika hospitali hiyo na Kituo cha Afya cha Makole zilikuwa zikiendelea kama kawaida.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk.  Ezeckiel Mpuya, alisema wameendelea na huduma za matibabu kama kawaida katika hospitali yao.

MGOMO BUGANDO WATHIBITISHWA

Uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Bugando ya jijini Mwanza umetihibitisha baadhi ya madaktari wake kuanza mgomo rasmi.

Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali hiyo, Dk. Japhet Gilyoma, ameliambia NIPASHE jana kuwa, licha ya mgomo huo kuanza, lakini hali ya huduma za matibabu bado si mbaya sana kwa sababu kuna madaktari bingwa ambao waliendelea kuhudumia wagonjwa juzi na jana.

“Ni kweli kwamba madaktari wetu pia wameingia katika mgomo, lakini kama unavyojua leo(jana ) ni weekend (mwisho wa juma) madaktari wanaokuwa zamu ni wachache, ninachoweza kusema kwa sasa ni kwamba hali ya matibabu si mbaya kwa sababu specialists (madaktari bingwa) wanaendelea na matibabu, ” alisema.

TANGA SHWARI

Katika Hospitali ya Mkoa wa Tanga  ya Bombo, jana madaktari waliokekana wakiwa wanatoa huduma za katibabu kwa wagonjwa kama kawaida.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...
 
Web Directories
PageHeat