StatsCrop - Free website analyzer!

Ads 468x60px

AddToAny

Lorem

Social Icons

June 25, 2012

KOMBANI: MISHAHARA HAITACHELEWA TENA

Tweeted this Like this, be the first of your Friends
OFISI ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, imesema hakutakuwapo tena ucheleweshaji mishahara kwa watumishi wapya kutokana na kufungwa kwa mfumo wa mawasiliano ya kompyuta kila taasisi ya umma.
Taarifa hiyo ilitolewa jana na Waziri wa ofisi hiyo, Celina Kombani, wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma kuhusu maadhimisho ya siku ya Utumishi wa Umma yanayoadhimishwa leo.

 Kombani alisema mfumo huo  utawezesha taarifa za watumishi wapya kufika na kufanyiwa kazi haraka na  ofisi ya utumishi, hivyo  kuziwasilisha taarifa zao hazina kwa ajili ya malipo yao.
Alisema kwa sasa kila taasisi ya Serikali nchini imefungiwa mfumo huo wa kompyuta, hivyo wanatakiwa kuingiza taarifa za wafanyakazi wao pale walipo kwa kutumia mtandao.

 “Sasa hivi ukiona mishahara inachelewa basi ujue taarifa za mtumishi aliyeajiriwa zimechelewa kufika utumishi, kwa kuwa zinatakiwa kufika kabla ya tarehe 15 kwa ajili ya kupeleka taarifa hazina ili waandae malipo mwisho wa mwezi,” alisema Kombani.

Mbali na mishahara kutocheleweshwa, huduma hiyo ya mtandao pia itasaidia kupunguza malimbikizo ya madeni kwa watumishi wa umma kwa kuwa taarifa za kila siku za mtumishi zitakuwa zikifika ofisi ya utumishi kwa wakati.

Taarifa hizo ni pamoja na kupandishwa vyeo kwa wafanyakazi, taarifa za vifo, kuachishwa kazi, likizo na taarifa za wafanyakazi wanaostaafu.

“Mfumo  huu toka umeanzishwa una miezi saba na umeonyesha mafanikio kwa kuwa kwa kiasi kikubwa, suala la malalamiko ya malimbikizo mbalimbali ya watumishi yamepungua ukilinganisha na awali. Tunategemea kuyamaliza kabisa hapo baadaye,” alisema.

Alisema Serikali imeunda Bodi ya Mishahara na Maslahi kwa Watumishi wa Umma, ambayo itakuwa na jukumu la kufanya utafiti juu ya hali ya mishahara ya watumishi wa umma.

Waziri Kombani alisema bodi hiyo itachunguza mishahara ya watumishi wa umma wote na kulinganisha na hali ya uchumi na gharama za maisha, itaanza kazi mwaka huu wa fedha.

Kuhusu maadhimisho ya Siku ya Utumishi wa Umma, Kombani alisema kaulimbiu ya mwaka huu  ni ‘Kujenga uwezo wa utekelezaji wa mkataba wa misingi na kanuni za utumishi wa umma na utawala, ili kuwa nchi inayojimudu kwa maendeleo Afrika’.

Alisema kama ilivyo kawaida kila mwaka kuadhimisha siku ya Utumishi wa Umma kwa kufanya maonyesho, mwaka huu hayakuwepo ikiwa ni moja ya utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kubana matumizi ya fedha za umma.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...
 
Web Directories
PageHeat