StatsCrop - Free website analyzer!

Ads 468x60px

AddToAny

Lorem

Social Icons

August 4, 2012

KIFO CHA MWANANGU BADO KINANIUMIZA

Tweeted this Like this, be the first of your Friends


HOLLYWOOD, MAREKANI
STAA, Sylvester Stallone Rambo, amemzika mtoto wake wa kwanza, Sage Stallone, ambaye alifariki baada ya kumeza madawa mengi.

Sage ambaye amewahi kuigiza na baba wake katika filamu ya Rocky V, alifariki dunia mapema mwezi huu ikiwa ni siku chache kabla ya kufunga ndoa.

Chanzo cha kifo chake hakijathibitishwa na daktari, isipokuwa maiti yake ilikutwa pembeni ya chupa tupu za vidonge zipatazo hamsini. Sage amefariki akiwa na umri wa miaka 36.

Kama alivyo baba yake, naye alikuwa mwigizaji, mwongozaji na mtayarishaji wa filamu.

Muswada binafsi kwa hati ya dharura: Marekebisho ya Sheria za Hifadhi ya Jamii

Tweeted this Like this, be the first of your Friends

Leo tarehe 03 Agosti 2012 kwa mujibu wa Kanuni ya 68 (7) ya Kanuni za Kudumu za Bunge na kwa kuzingatia kuwa marekebisho yamefanyika kwenye ratiba ya bunge ambapo Mkutano wa Bunge sasa umepangwa kuahirishwa tarehe 16 Agosti 2012 na hoja za wabunge zimeondolewa kwenye ratiba.

Nimeomba muongozo ama Serikali itoe kauli bungeni ya kutengua tangazo lililotolewa na Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) ili kuwezesha mafao ya kujitoa kuendelea kutolewa au uongozi wa Bunge uruhusu niwasilishe muswada binafsi wa sheria kwa hati ya dharura tarehe 16 Agosti 2012 kwa ajili ya kufanya marekebisho kwenye sheria husika ili kuruhusu mafao ya kujitoa kuendelea kutolewa.

Pamoja na hatua hiyo ya kuomba muongozo nimechukua hatua ya ziada ya kumwandikia Katibu wa Bunge kumweleza kusudio la kuwasilisha Muswada Binafsi juu ya Marekebisho ya Sheria za Hifadhi ya Jamii (The Social Security Laws (Ammendments) Act wa mwaka 2012 kwa hati ya dharura kwa mujibu wa Kanuni ya 81 ya Kanuni za Kudumu za Bunge (Toleo la Mwaka 2007).



Lengo la Muswada huo ni kufanya marekebisho yenye kuwezesha kurejeshwa kwa fao la kujitoa (withdrawal benefits) ili kuruhusu kuendelea kutolewa kwa mafao kwa mwanachama wa mfuko ya hifadhi ya jamii anapoacha kazi na kuhitaji kupewa mafao yake kabla ya kufikisha umri wa kustaafu kwa hiari (miaka 55) au kwa lazima (miaka 60) au pale anapopata ulemavu wa kudumu.

Nimeomba kupatiwa ushauri na usaidizi wa kisheria kwa mujibu wa Kanuni ya 21 (1) (d), (e) na (2) ili kuweza kuandaa Muswada Binafsi wa Sheria kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (1), Taarifa ya Muswada huo kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (2), hati ya kuwasilisha muswada kwa dharura na hoja ya kutengua masharti kuhusu muda wa utangazaji wa Miswada ya Sheria kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (5) ya Kanuni za Kudumu za Bunge (Toleo la Mwaka 2007).

Kwa mujibu wa Kanuni ya 81 (5) masharti kuhusu muda wa utangazaji wa Miswada ya Sheria yanaweza kuwekwa kando na kutenguliwa kwa hoja kutolewa na kuamuliwa kama kutawasilishwa Bungeni hati iliyowekwa saini na theluthi mbili ya Wajumbe wote wa Kamati kama ni Muswada wa Kamati na kwa Muswada wa Mbunge hati iliyowekwa saini na Wabunge wasiopungua kumi inayoeleza kuwa muswada binafsi uliotajwa katika hati hiyo ni wa dharura.

Naomba kutoa taarifa kwamba kuanzia jumatatu tarehe 6 Agosti 2012 nitaanza kukusanya saini za wabunge wanaounga mkono kuwasilishwa kwa muswada tajwa kwa hati ya dharura kufanya haraka marekebisho yenye kuwezesha kurejeshwa kwa fao la kujitoa (withdrawal benefits) ili kuruhusu kuendelea kutolewa kwa mafao kwa mwanachama wa mfuko ya hifadhi ya jamii.

Nimeomba pia kwa Katibu wa Bunge kwa mujibu kifungu cha 10 cha Sheria ya ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge Cap 296 R.E 2002 kupatiwa nakala ya taarifa na nyaraka zifuatazo kwa ajili ya kujiandaa kuwasilisha muswada husika: Social Security Ammendment Act no.5 ya mwaka 2012, Sheria za Hifadhi ya Jamii zinazohusika, Taarifa na mapendekezo yaliyowasilishwa na kupelekea kufutwa kwa mafao ya kujitoa (withdrawal benefits) na maelezo kuhusu hatua ambayo kifungu husika kiliingizwa na hatimaye kupitishwa na Bunge tarehe 13 Aprili 2012.

Pamoja na kuomba taarifa na nyaraka kupitia kwa Katibu wa Bunge natoa mwito kwa wadau wa mifuko ya hifadhi ya jamii kutunipatia maoni na mapendekezo kwa ya kuzingatiwa kwenye Muswada Binafsi wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Sheria za Hifadhi ya Jamii (The Social Security Laws (Ammendments) Act wa mwaka 2012 katika kipindi cha wiki moja.

Ikumbukwe kwamba kifungu cha kufuta mafao ya kujitoa kilichozua mgogoro hakikuwepo wakati muswada uliposomwa kwa mara ya kwanza bungeni tarehe 1 Februari 2012 bali kiliwasilishwa kupitia jedwali la marekebisho ya Wizara lililowasilishwa tarehe 13 Aprili 2012 bila malengo na madhumuni yake kuelezwa kwa ukamilifu.

Kupitishwa kwa kifungu hicho kumethibitisha maneno niliyoyatoa bungeni kuwa tumefika hapa tulipo kutokana na ‘uzembe wa bunge na wabunge’ na kwa hili pamoja na mchango nilioutoa bungeni kwa maandishi siku hiyo juu ya haja ya kuwa mfumo mpana zaidi wa pensheni na hifadhi ya jamii (universal pension and social security) pamoja na kuwa sikuunga mkono kifungu husika kilichoingizwa kinyemela naomba radhi kwa wananchi wa Ubungo na wafanyakazi kwa kutokuwasilisha jedwali la marekebisho kupinga kifungu hicho kuingizwa.

Izingatiwe kuwa ili kurekebisha hali hiyo tarehe 27 Julai 2012 kwa nafasi yangu ya Waziri Kivuli wa Nishati na Madini kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani niliitaka Serikali itoe maelezo maelezo kuhusu taarifa zilizotolewa bungeni tarehe 13 Aprili 2012 kuwa wafanyakazi ikiwemo wa migodini kupitia vyama vyao walihusishwa kutoa maoni yaliyopelekea kufutwa kwa fao la kujitoa (withdrawal benefits); suala ambalo Chama Cha Wafanyakazi wa Migodini (TAMICO) kililikanusha.

Hata hivyo, Waziri wa Nishati na Madini wakati wa majumuisho ya Hotuba yake tarehe 28 Julai 2012 hakutoa majibu yoyote bungeni kuhusu suala hilo hali ambayo imesababisha migongano kuendelea katika migodi mbalimbali kuhusu madai hayo hali ambayo kwa taarifa nilizozipata tarehe 1 na 2 Agosti 2012 inaweza kusababisha migomo migodini. Kufutwa kwa fao la kujitoa kumelalamikiwa pia na wafanyakazi na wadau wa hifadhi ya jamii katika Jimbo la Ubungo na katika taifa kwa ujumla.

Hata hivyo, suala hili na tukio husika litumike kama rejea ya bunge na wabunge kuikatalia Serikali kuwasilisha marekebisho yenye athari kubwa kipindi cha mwisho na hivyo wabunge kukosa fursa ya kupata maoni ya wananchi na pia Serikali itakiwe kuomba radhi kufuatia kulipotosha bunge kuwa wadau wa hifadhi ya jamii hususan wafanyakazi na vyama vyao walishirikishwa na kuridhia wakati ambapo wamejitokeza na kukanusha madai hayo yaliyotolewa na Wizara bungeni.

Kwa upande mwingine kufutwa kwa mafao ya kujitoa msingi wake haupo kwenye marekebisho ya sheria yaliyofanyika tarehe 13 Aprili 2012 pekee bali ni udhaifu katika mfumo mzima wa kisera na kisheria wa hifadhi ya jamii nchini hali ambayo inahitaji wadau kutaka mabadiliko makubwa.

Hivyo, naungana na wote wenye kutaka Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) kutengua taarifa kwa umma iliyotolewa ya kueleza kuwa “kufuatia kuanza kutumika kwa Sheria hiyo (ya 13 Aprili 2012) maombi mapya ya kujitoa yamesitishwa kwa kipindi cha miezi sita hadi pale miongozo itakapotolewa ili kuwezesha Mamlaka na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kutoa elimu kwa Wadau”.
Aidha, pamoja na Mamlaka kueleza kwamba sitisho la fao la kujitoa si kwa sababu za Kiserikali au Mifuko kufilisika ni vizuri mamlaka ikaeleza kwa uwazi na ukweli sababu zingine za kufanyika kwa marekebisho hayo zaidi ya ile ya kutimiza malengo ya Hifadhi ya Jamii ambayo ni kuhakikisha kuwa Mwanachama anapostaafu anapata mafao bora yatakayomwezesha kumudu hali ya maisha ya uzeeni. Tahadhari za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika taarifa za Hesabu za mwaka 2010/2011 na miaka mingine zinaashiria masuala ya ziada ambayo yanaweza kuwa yameisukuma Serikali kuja na mbinu zingine za kuhakikisha uendelevu wa mifuko ikiwemo kupitia marekebisho ya sheria za hifadhi ya jamii.

Ili bunge liweze kutimiza wajibu wa kuishauri na kuisimamia serikali kufanya marekebisho yanayostahili ya sheria husika kwa haraka ni muhimu ratiba ya bunge ikabadilishwa.

Tafsiri ya marekebisho ya ratiba yaliyofanyika ni kuwa hoja binafsi niliyoiwasilisha kwa katibu wa Bunge kutaka bunge lijadili na kupitisha maazimio ya hatua za haraka za kuboresha upatikanaji wa majisafi na ushughulikiaji wa majitaka haitapata nafasi ya kujadiliwa bungeni. Aidha ratiba hiyo mpya hoja binafsi iliyoelezwa kuwa itawasilishwa na Mbunge wa Kisarawe Seleman Jafo kuhusu kufutwa kwa mafao ya kujitoa kufuatia marekebisho ya sheria za Hifadhi za Jamii nayo haitawasilishwa kwenye mkutano huu wa Bunge unaoendelea kama ratiba haitafanyiwa marekebisho.

Hata hivyo, izingatiwe kuwa chanzo cha kufutwa kwa mafao ya kujitoa ni marekebisho ya sheria za hifadhi ya jamii hivyo ufumbuzi wa kurejesha fao la kujitoa unapaswa kuwa ni marekebisho ya sheria hatua ambayo njia ya haraka ya kuifikia ni kuwasilishwa kwa muswada wa sheria ama na serikali au kamati au mbunge badala ya hoja binafsi.

Hoja binafsi inaweza kuwezesha bunge kujadili na kupitisha maazimio ya kuitaka Serikali kuwasilisha marekebisho ya sheria au kuishauri na kuisimamia serikali na mamlaka zake katika utekelezaji wa sheria lakini sheria itaendelea kuwa palepale mpaka marekebisho yatakapofanywa kwa kuwasilishwa muswada wa sheria hatua ambayo nimeamua kuanzisha mchakato wa kuwezesha ichukuliwe.

Wenu katika kuwawakilisha wananchi,

John Mnyika (Mb)


03/08/2012

HUU NDIO MKOKO MPYA WA NGASA ALIOPEWA NA SIMBA

Tweeted this Like this, be the first of your Friends Hapa Ngasa akiwa ndani ya mkoko wake mpya aliopewa na Simba

 
Huu ndio mkoko mpya aliopewa Ngasa unavyoonekana kwa mbele
 
Baadhi ya mashabiki wa Simba wakimchungulia Ngasa alipokuwa ndani ya mkoko wake

OFISI YA TAIFA YA TAKWIMU YATOA TAARIFA YA HALI YA UCHUMI , PATO LA TAIFA LA TANZANIA LAKUA

Tweeted this Like this, be the first of your Friends
pato la taifa lakua from national bureau of statistcs
Mkurugenzi wa Takwimu za Uchumi wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Bw. Morrice Oyuke akiongea na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam kuelezea hali ya Ukuaji wa Pato la Taifa kwa 7.1% katika kipindi cha robo mwaka 2012.(Picha na Aron Msigwa – MAELEZO).
Na. Aron Msigwa – MAELEZO.
Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) imetoa taarifa ya hali ya uchumi nchini na kufafanua kuwa  pato la taifa  la Tanzania limekua kwa  asilimia 7.1 katika kipindi cha robo ya mwaka 2012  ikilinganishwa  na asilimia 6.1  za mwaka jana.
Ukuaji huo wa asilimia 7.1 unatokana na ongezeko la uzalishaji katika shughuli mbalimbali za kiuchumi zikiwemo za kilimo, Uvuvi, Viwanda, Ujenzi na zile za utoaji wa huduma mbalimbali za jamii.
Akitoa taarifa hiyo leo jijini Dar es salaam Mkurugenzi wa Takwimu za Uchumi wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Bw. Morrice Oyuke amesema kuwa lengo la  utoaji wa taarifa hizo kwa vipindi vifupi vya vya  robo mwaka unalenga kuwapatia wadau wa Takwimu za Pato la Taifa uwezo wa kutathmini mabadiliko ya ukuaji wa uchumi nchini. 
Amesema kuwa jumla ya thamani ya pato la Taifa katika kipindi cha robo ya mwaka 2012 ni shilingi 4,220,535 milioni ikilinganishwa na kiasi cha shilingi milioni 3,940,261 za mwaka 2011.
Amefafanua kuwa ukuaji wa shughuli uzalishaji katika shughuli za kilimo nchini ulifikia asilimia 1.4 katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka 2012 zikilinganishwa na asilimia 1.2 katika kipindi hicho kwa mwaka 2011 kutokana na upatikanaji wa mvua za kutosha nchini katika mikoa inayozalisha mazao kwa wingi.
 Amesema ukuaji katika shughuli za uvuvi ulikua  asilimia 2.6 katika robo ya kwanza ya mwaka 2012 huku shughuli za uchumi katika sekta ya viwanda na Ujenzi ambayo inahusisha uchimbaji wa madini na kokoto ikikua kwa asilimia 14.3 ikilinganishwa na 0.8% za mwaka 2011.
Bw. Oyuke ameongeza kuwa ongezeko hilo  la uzalishaji wa madini ya dhahabu linatokana na uzalishaji wa wa madini ya dhahabu kutoka kilo 8,140 kwa mwaka 2011 hadi kufikia kilo 16,736 kwa mwaka 2012.
Pia amebainisha kuwa  shughuli za utoaji wa huduma za biashara za jumla na rejareja, ukarabati wa magari na pikipiki na vifaa vingine vya majumbani katika kipindi hicho zilifikia asilimia 9.0 huku shughuli za upangishaji nyumba na biashara zikiwa 8.2 %, uchukuzi na mawasiliano 16.4%, hoteli na migahawa 3.8%, Benki asilimia 15 shughuli za uendeshaji  serikali 6.4%, Elimu 6.1% na utoaji wa huduma za Afya nchini zikikua kwa kasi ya asilimia 5.1.

August 3, 2012

Taswira Mbalimbali Kutoka Maonyesho ya Wakulima Nanenane Mkoani Dodoma

Tweeted this Like this, be the first of your Friends
 Mtunzaji Kumbukumbu na Mhasibu Abbas Mnyeto wa Wizara ya Fedha wakiwasaidia wazee wastafu upande wa Kilimo juu ya taratibu za kupata pesheni kwa watumishi wanapostaafu jana mjini Dodoma walipokuwa kwenye banda la Wizara hiyo kwenye maonyesho ya wakulima nanenane.
  Afisa Malipo ya Pesheni wa Mfuko wa Pesheni kwa watumishi wa umma (PSPF) Andrew Dayson (kushoto) akiwasidia Maafisa Polisi kujua kiwango michango yao mbalimbali ambayo wamekwishachangia tangu waingie katika utumishi wa umma wakati walipotembelea banda la Wizara ya Fedha kwenye maonyesho ya wakulima ya nanenane jana mjini Dodoma.
 Kaimu Afisa Uhusiano wa wa Mfuko wa Pesheni kwa watumishi wa umma (PSPF) Hawa Kikeke(kushoto) na Afisa Malipo ya Pesheni wa Mfuko wa Pesheni kwa watumishi wa umma (PSPF) Andrew Dayson (wa pili kutoka kushoto) wakiwasaidia Maafisa wa Polisi juu ya kupata taarifa za michango yao mbalimbali ambayo wamekwishachangia tangu waingie katika utumishi wa umma wakati walipotembelea banda la Wizara ya Fedha kwenye maonyesho ya wakulima ya nanenane jana mjini Dodoma.
 Afisa Uhusiano wa Chuo Mipango Dodoma Sarah Mmari (kushoto) akimwelimisha Yulis Otto (kulia) utaratibu wa kujiunga na masomo katika Chuo hicho wakati mzee huyo alioptembelea banda la Wizara ya Fedha jana katika maonyesho yanayoendelea mjini Dodoma.
 Afisa Uhusiano wa Chuo Mipango Dodoma Sarah Mmari (kushoto) akimwelimisha Yulis Otto (kulia) utaratibu wa kujiunga na masomo katika Chuo hicho wakati mzee huyo alioptembelea banda la Wizara ya Fedha jana katika maonyesho yanayoendelea mjini Dodoma.
 Afisa Masoko kutoka Dhamana ya Uwekezaji Tanzania (UTT) Said Mkomwa(kulia) akiwaelimisha wananchi faida za kuwekeza katika mifuko iliyoanzishwa na Dhamana ya Uwekezaji Tanzania jana mjini Dodoma walipotembelea banda la Wizara hiyo kwenye maonyesho ya wakulima nanenane.
 Mwanasheria kutoka Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana Emilia Mkubulo(kulia) akimwelimisha mmoja wa wananchi faida za kununua hisa jana mjini Dodoma alipotembelea banda la Wizara hiyo kwenye maonyesho ya wakulima nanenane.
 Afisa Uendeshaji wa Mfuko wa Pesheni kwa watumishi wa umma (PSPF) Kahenga Maulid( wa pili kutoka kulia) na Afisa Malipo ya Pesheni wa Mfuko wa Pesheni kwa watumishi wa umma (PSPF) Andrew Dayson (wa pili kutoka kushoto) wakiwasaidia watumishi wa Chuo kikuu cha Dodoma (UDOM) Monica Kung’aro (kushoto) na Mary Kulwijila(kulia) juu ya kupata taarifa za michango yao mbalimbali ambayo wamekwishachangia tangu waingie katika utumishi wa umma wakati walipotembelea banda la Wizara ya Fedha kwenye maonyesho ya wakulima ya nanenane jana mjini Dodoma.

Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) Chasitisha Mgomo Nchi Nzima

Tweeted this Like this, be the first of your Friends
 Rais Chama cha Walimu nchini (CWT) Mwl. Gratian Mukoba akitoa taarifa ya chama hicho
--
UONGOZI wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT), umesitisha mgomo uliokuwa unaendelea nchini, hivyo kuwataka walimu kurejea kazini.
Rais wa chama hicho, Mukoba amesema wameamua kusitisha mgomo, baada ya kuingiwa na hofu ya viongozi wao wa juu kuhofiwa kukamatwa.

EBSS Dar es Salaam vipaji kibao

Tweeted this Like this, be the first of your Friends
Ikiwa imeingia katika siku ya pili ya usaili wa Epiq BSS Dar-es-Salaam ambao unafanyika Coco Beach jijini hapa vijana wengi wamezidi kujitokeza kutoka maemneo mbalimbali ya jiji kusaka nafasi ya kushiki katika shindano hilo kubwa hapa nchini la kuibua vipaji vya wasanii wa muziki. Hadi jana usiku majira ya saa moja zaidi ya vijana mia tatu bado walikuwa katika foleni ya kutaka kuonana na majaji kwaajili ya usaili.
 Jaji Mkuu wa Shindano la EBSS Ritta Poulsen ‘Madam Ritta’ akitafakari jambo wakati akimsikiliza mmoja wa washiriki waliojitokeza katika usaili.
 Mmoja wa washiriki wa EBSS katika mchujo wa Dar es Salaam akichangia damu
 Maofisa kutoka kitengo cha Damu Salama wakiendelea na shughuli ya kutoa maelezo na kupima damu kwa vijana waliojitokeza katika zoezi la  uchangiaji damu kwa washiriki wa EBSS jijini Dar es Salaam.
 Mwanamuziki Banana Zorro nae alikuwepo Coco Beach katika usaili wa EBSS yeye hakuwa mshiriki bali alifika kutoa sapoti kwa jopo la majaji na vijana wanaoshiriki.
 Hakuna kazi rahisi hata siku moja, na hapa jamaa wakiuchapa usingizi baada ya kusubiri sana zamu yao ifike na kuweka sawa mistari yao.
 Foleni ya washiriki waliokuwa wakisubiri kuonana na majaji katika usaili wa EBSS katika fukwe ya bahari ya Hindi eneo la Coco Beach Dar es Salaam.
Hizi ni swaga za kuondokea , jamaa akitoka ndani baada ya kuonana na majaji

BREAKING NUUZ: AJALI MBAYA YATOKEA HIMO ASUBUHI HII

Tweeted this Like this, be the first of your Friends
 BAADHI YA MAJERUHI WALIOPATA MAJERAHA MADOGO WAKIPATA HUDUMA KATIKA HOSPITALI YA KCMC LEO ASUBUHI
 MAJERUHI AKIKIMBIZWA ICU KUPATA HUDUMA ZAIDI

GARI ZA JESHI LA POLISI ZIKIWA ZIMEPAKI NJE YA CASUALITY KCMC ASUBUHI HII BAADA YA MAJERUHI HAO KUFIKISHWA HOSPITALINI HAPA

Ajali hiyo mbaya imeripotiwa kutokea eneo la himo asubuhi hii na imehusisha gari aina ya canter. Habari zaidi tutazipata baadae baada ya madaktari wa KCMC na polisi Mkoa wa kilimanjaro kutoa taarifa rasmi.

RAIS KIKWETE ATOA NG’OMBE 1500 KWA WANANCHI WILAYA TATU ARUSHA KILA MWEZI.

Tweeted this Like this, be the first of your Friends


Rais  Jakaya Mrisho kikwete akizindua mpango wa kugawa Ng’ombe 1500 kila mwezi kwa wananchi wa wilaya tatu za Mkoa wa Arusha kama kifuta jashp cha kupoteza kiasi cha mifugo 800,000 kutokana na ukame na athari zake mwaka 2008/2009.


Rais Jakaya Kikwete akimkabidhi Ng’ombe mmoja wa wakaazi wa Monduli walioathririka na na ukame mwaka 2008/2009 ambapo walipoteza mifugo yao yote. Hafla hii imefanyika leo Monduli.



Rais Jakaya Kikwete akiwahutubia wananchi wa kijiji cha Makuyuni,Wilayani Monduli mchana wa leo wakati alipofika kuzindua mpango wa kugawa ng’ombe 1500 kila mwezi kwa wananchi wa wilaya tatu za Mkoa wa Arusha kama kifuta jasho cha kupoteza kiasi cha mifugo 800,000 kutokana na ukame na athari zake mwaka 2008/2009.


Rais Jakaya Kikwete akisalimiana na Wananchi wa kijiji cha Makuyuni,Wilayani Monduli leo wakati alipofika kuzindua mpango wa kugawa ng’ombe 1500 kila mwezi kwa wananchi wa wilaya tatu za Mkoa wa Arusha kama kifuta jasho cha kupoteza kiasi cha mifugo 800,000 kutokana na ukame na athari zake mwaka 2008/2009.(Picha na Ikulu).


SERIKALI itakuwa inagawa ng’ombe 1500 kila mwezi kwa wananchi wa wilaya tatu za Mkoa wa Arusha kama kifuta jasho cha kupoteza kiasi cha karibu mifugo 800,000 iliyopotea kutokana na ukame na athari zake mwaka 2008/2009.

Ahadi hiyo imetolewa leo, Alhamisi, Agosti 2, 2012 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete wakati alipozindua Mradi wa Serikali wa Uwezeshaji Mifugo kwa waliopotelewa mifugo yote katika Wilaya ya Monduli kwenye sherehe iliyofanyika Makuyuni wilayani humo. 

Katika uzinduzi huo uliohudhuriwa na viongozi wa Mkoa wa Arusha wakiwemo wakuu wa wilaya na wabunge wa mkoa huo, Rais Kikwete amegawa ng’ombe 500 kwa kundi la kwanza la wananchi ikiwa ni mitamba minne na dume moja la kisasa kwa kaya 16 za mwanzo. 

Uzinduzi huo ni wa pili kufanywa na Rais Kikwete chini ya Mradi huo wa kwanza wa aina yake kubuniwa na Serikali katika historia na wenye thamani ya sh. Bilioni 12.9.

Februari 19, mwaka huu, Rais Kikwete alizindua Mradi kama huo katika Wilaya ya Loliondo kwenye sherehe zilizofanyika mjini Loliondo.

WIZARA YA FEDHA YASHIRIKI MAONYESHO YA NANENANE MJINI DODOMA.

Tweeted this Like this, be the first of your Friends
Ofisa kutoka Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha Thabit Matotola (wa pili kushoto) akiwaelimisha wananchi leo majukumu ya Wizara hiyo kwenye maonyesho ya wakulima nanenane mjini Dodoma.
Ofisa kutoka Dhamana ya uwekezaji Tanzania(UTT) Mvumo Balati (kushoto) akiwaelimisha Polisi faida kuwekeza katika mfuko huo leo mjini Dodoma wakati walitembelea maonyesho ya nanenane mjini Dodoma kwenye banda la Wizara ya Fedha.
Ofisa Operesheni wa Mfuko wa Pesheni ya Watumishi wa Umma (PSPF) Kahenga Maulid (kushoto)akijibu maswali mbalimbali ya mwananchi huyo aliyetaka kujua majukumu ya mfuko katika kumsaidia mtumishi umma wakati wa maonyesho ya wakulima ya nanenane mjini Dodoma leo.
 Afisa Maendeleo ya Jamii Mwandamizi wa Idara ya Kuondoa Umaskini William Ghumbi (KUSHOTO) akiwaelimisha wananchi juu ya MKUKUTA II walipotembelea  banda la Wizara ya Fedha leo mjini Dodoma kwenye maonyesho ya nanenane .(Picha na HAZINA-Dodoma).

ASHITAKIWA BAADA YA MKONO WAKE KUNYOFOLEWA NA MAMBA.

Tweeted this Like this, be the first of your Friends

HAKIELIMU WAISHAURI SERIKALI, CWT KUHUSU MGOMO WA WALIMU.

Tweeted this Like this, be the first of your Friends

Meneja wa Kitengo cha Habari na Ushauri, HakiElimu, Nyanda Shuli (kushoto) akijibu maswali anuai ya wanahabari katika mkutano huo.
Meneja wa Kitengo cha Habari na Ushauri, HakiElimu, Nyanda Shuli akifafanua jambo kwa waandishi wa habari.
Mkutano ukiendelea na wanahabari.
Na Joachim Mushi, Thehabari.com
Tasisi ya HakiElimu nchini imeishauri Serikali pamoja na Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) kufikia makubaliano haraka iwezekanavyo, ili kumaliza mgomo uliopo kwani waathirika zaidi na mgomo huo si wao bali ni ni wanafunzi.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa HakiElimu, Bi. Elizabeth Missokia alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusiana na mgomo wa walimu unaoendelea maeneo mbalimbali nchini.
Alisema kila mwanafunzi ana haki ya kujifunza na kuelimishwa, kitu ambacho hawakipati kwa sasa kutokana na mgomo wa walimu wanaoshinikiza Serikali iwaongeze mishahara pamoja na kuwaboreshea mazingira ya kazi zao.
Mkurugenzi huyo alisema kauli ya Serikali kudai haina uwezo wa kuboresha maslahi na mazingira ya kazi ya  watumishi wake haileti unafuu wa maisha kwa watumishi wa umma hivyo kushauri iangalie namna ya kufanya kumaliza mgogoro huo.
“HakiElimu inasisitiza kwamba nchi itafanikiwa kuboresha elimu endapo tu itawekeza kwa walimu kwa kuboresha mazingira ya kazi, maslahi ya walimu, kuwashirikisha walimu katika maamuzi kuhusu masuala ya elimu  na kuwapa walimu mafunzo kazini. Elimu bora haiwezi kuletwa na walimu walio hoi,” alisema Missokia.
Aidha amewataka walimu kuhakikisha wanadai haki zao huku wakiendelea kuwajibika kwa kufundisha na kuendeleza elimu yetu, kwani wanamgogoro na Serikali na wala si wanafunzi na jamii kwa ujumla.
“HakiElimu inawakumbusha walimu kuwajibika. Wadai haki zao, huku wakitimiza wajibu wao wa kufundisha na kuendeleza elimu yetu. Wafundishe kwa bidii bila kinyongo, kwa kuwa wasipowajibika watakuwa wanawaumiza wanafunzi na jamii kwa ujumla. Mgogoro uliopo ni baina yao na Serikali, na si wanafunzi,” alisema Mkurugenzi huyo Mtendaji.
“Viongozi wa Serikali wasiwabeze walimu; kwa kufanya hivyo wanawakatisha tamaa. Hata kama baadhi ya walimu hawakusoma kwa miaka mingi kama ilivyo kwa fani nyingine, wana umuhimu mkubwa sana. Ndio wanaowaandaa watanzania wa leo na kesho kimtazamo na kimaarifa. Hivyo, kudai kuboreshewa mazingira ya kazi ni haki yao; na Serikali inaweza kutimiza wajibu wake kwa kuwasikiliza na kushauriana nao bila ubabe na kejeli,” alisema.
Pamoja na hayo ameliomba Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuingilia kati mgogoro huo na kutenga muda kujadili suala hilo kwa kina ikiwa ni pamoja na kuishauri serikali, hasa kuhusu tahadhari za kuchukua ili tatizo kama hili lisitokee tena.
“Bunge lina wajibu wa kuishauri na kuisimamia Serikali kuhusu sera, utendaji na usimamizi wa elimu nchini. Inasikitisha kwamba Bunge linakwepa kujadili tatizo hili kwa maelezo kwamba liko mahakamani. Tunaamini kwamba mahakama italiangalia suala hili na kutenda haki, lakini wajibu wa Bunge uko pale pale…” alisema Bi. Missokia.
Amekiri kwamba ni kweli gharama za maisha zinazidi kupanda, huku mfumuko wa bei nao unaendelea kuwaumiza watumishi kila siku, hivyo kuishauri Serikali kutafuta vyanzo mbadala vya mapato ili kuweza kuwaboreshea mapato watumishi wake.
“Serikali ijijengee utaratibu wa kuboresha mazingira ya watumishi wake, na si kusubiri kwenda mahakamani kuzuia watumishi kugoma. Watumishi wa umma watafanya kazi kwa ari endapo tu wameridhika na mazingira ya kazi na maslahi yao; na si kwa kutumia uamuzi wa mahakama peke yake.”
Habari hii imeandaliwa na Mtandao wa Thehabari.com (www.thehabari.com)

August 2, 2012

MAKAMU WA PILI WA RAIS ZANZIBAR AZINDUA SHULE YA URAFIKI

Tweeted this Like this, be the first of your Friends
Na Salama Thalaba,
Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar,Balozi Seif Ali Idd leo amezindua ujenzi wa Skuli ya msingi iliyopewa jina la Urafiki inayofadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China.
 
Balozi Seif Idd aliyasema hayo katika skuli ya Mwanakwerekwe C wakati akizindua ujenzi wa skuli ya urafiki inayofafdhiliwa  na Serikali ya China kwa Dola za Marekani 1.6.
katika sherehe za uzinduzi wa Skuli hiyo yenye madarasa kumi na mbili,Makamu wa Rais amesema kwamba wananchi wa Zanzibar wanathamini mchango unaotolewa na Serikali ya China.
Pia alisema Serikali inaupa kipaumbele sana mchango huo kwa kuchangia katika sekta ya Elimu kwani bila ya elimu hakuna maendeleo.
Aidha, Balozi Seif Idd amesema kwamba Serikali itachukua kila jitihada kuhakikisha tatizo la vikalio linamalizika katika skuli zote za Unguju na Pemba alisema.
 Utoaji wa madeksi hayo

Mbali na ujenzi wa Skuli hiyo, pia Serikali ya China kupitia Jimbo la Sichuan imetoa jumla ya madawati 480 kwa ajili ya Skuli mbalimbali za Unguja.
Kwa upande wake, Balozi mdogo wa China Zanzibar, Chen Qiman alisema Serikali ya China itaendelea kuisaidia Zanzibar katika nyanja mbalimbali.
Ameipongeza Serikali kwa juhudi inazochukuwa kutekeleza mipango yake mbalimbali ya kuwalatea maendeleo wananchi wa Zanzibar akitoa mfano suala zima la elimu.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali,Ali Juma Shamuhuna ameipongeza Serikali ya China kwa msaada wao kwa Wizara ya elimu hasa ujenzi wa Skuli hiyo pamoja na msaada wa madawati.
 
source: fullshangwe blog

MISS MWANZA KUFANYIKA AGOSTI 31

Tweeted this Like this, be the first of your Friends
Mrembo wa mkoa wa Mwanza 2012/13 atapatikana ijumaa ya agosti 31 katika viwanja vya Yatch Club Mwanza.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na muaandaji wa kampuni ya Sisi Entertainment John Doto, amesema shindano hilo linalovuta hisia za wengi ndani ya mkoa wa Mwanza na kanda ya ziwa kwa ujumla, litashirikisha warembo tariban 20 kutoka wilaya zote za mkoa Mwanza.


John Doto amesema warembo wote watakaa kambini kwa wiki mbili, ambapo kambi rasmi itaanza tarehe 20 agosti mwaka huu katika hoteli ya Isamilo Lodge. Shindano la Redds Miss Mwanza 2012/13, lilisogezwa mbele kufuatia mwezi mtukufu wa Ramadhani.


Wakiwa kambini warembo watapata fursa ya kujifunza Mitembeo, Tabasamu, ufahamu wa kujieleza pamoja na kuvumbua vipaji mbalimbali.


John Dotto pia amesema warembo watakua na ziara ya kwenda kwenye mbuga za wanyama Serengeti, kutoa misaada kwa watoto yatima, vikongwe pamoja na kufanya usafi kwenye moja

ya Hospitali Jijini Mwanza na moja ya barabara za Mwanza.

Kwa miaka ya hivi karibuni, Mkoa wa Mwanza umekua ukitoa warembo wanaofanya vizuri mashindano ya Taifa.


Itakumbukwa Mwaka 2008 Nasreem Karim na Mwaka 2009 Miriam Gerald waliweza kushika Mataji ya Miss Tanzania wakitokea mkoa Mwanza.

August 1, 2012

MHE. ZITTO ASEMA TUHUMA ZILIZO ELEKEZWA KWAKE ZA RUSHWA NI SHINIKIZO LA KISIASA

Tweeted this Like this, be the first of your Friends


MBUNGE WA KIGOMA KASKAZINI, NAIBU KATIBU MKUU (CHADEMA) ZITTO KABWE

Ndugu Waandishi,
Nalazimika kukutana nanyi kutoa maelezo juu ya tuhuma zenye shinikizo la kisiasa zinazoelekezwa kwangu binafsi kwamba hata mimi nimeshiriki katika vitendo vya rushwa, kwa nafasi yangu kama Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mashirika ya Umma. Taarifa hizo, kama kawaida ya uzushi mwingine wowote zimesambazwa kimkakati na kwa kasi kubwa kiasi cha kuukanganya umma.
Nafahamu nabeba dhamana kubwa ya uongozi, taswira yangu ya uongozi daima imeakisi njozi na matumaini ya wananchi wa Kigoma Kaskazini, wananchi wanyonge na vijana kote nchini bila kujali itikadi zao za kisiasa, jinsia zao, makabila yao na rika zao. Hivyo, nawajibika kupitia kwenu kuwatoa hofu juu ya hisia potofu zinazopandikizwa kwao na wale wasiopenda kuona baadhi yetu tukiwaunganisha na kuwasemea watanzania wasio na sauti, dhidi ya vitendo vya hujuma na vyenye dhamira ovu kwa taifa.
Mkakati huo wa kuniunganisha na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanaotuhumiwa kwa kupokea Rushwa unatekelezwa kwa njia zifuatazo:-
  1. Kumekuwa na kauli za watendaji wa serikali ambao wamekuwa wakizieneza na hususan kutoa taswira kwamba baadhi ya kauli zangu zinatokana na ushawishi wa rushwa;
  2. Kuna taarifa ambazo zimeandikwa tena katika kurasa za mbele za baadhi ya vyombo vya habari zikidai ’’Zitto kitanzini’’ ama ’’Zitto sawa na popo nundu’’ zikiashiria kwamba na mimi ni mla rushwa; na
  3. Waandishi wa habari na jamii kwa ujumla wamefikia kuaminishwa habari hizi kiasi cha wengine kuuliza kwa nini Mhe. Zitto Kabwe hakutajwa katika orodha iliyotolewa na Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani.
Ndugu Waandishi,
Naomba kutoa ufafanuzi wa hicho kinachoelezwa kwamba nina ushiriki katika masuala ya rushwa hususan kwenye masuala yanayohusu sekta ya Nishati na Madini:-
  1. Mara baada ya bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Usambazaji wa Umeme Tanzania (TANESCO) chini ya Uenyekiti wake Meja Jenerali Mstaafu Robert Mboma kutangaza kwamba imemsimamisha kazi Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Nd. William Mhando ili kupisha uchunguzi wa baadhi ya vitendo/mwenendo wake, Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) ambayo mimi ni Mwenyekiti wake ilimuandikia Mhe. Spika kumuomba aridhie ili Kamati iweze kuwaita Bodi ya TANESCO, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu ya Serikali (CAG) na pia Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kujiridhisha na tuhuma zote zinazotajwa zinafanyiwa uchunguzi wa kina na hatua kuchukuliwa;
  2. Kamati ya POAC ninayoiongoza ilimuomba Mhe. Spika kuwaita wahusika tajwa kwa kuwa zilikuwapo tetesi kuwa kusimamishwa kazi kwa Mkurugenzi huyo siku chache kabla ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kulikuwa na lengo la kufunika ’madudu’ makubwa zaidi kwa kulichagiza Bunge na tukio hilo dogo, mkakati ambao naona umefanikiwa sana. Isitoshe, Kamati kutaka kujiridhisha na hatua za Bodi ni sehemu ya msingi ya utekelezaji wa majukumu ya Kamati yaliyowekwa kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge na pia Shirika la TANESCO ni moja kati ya mashirika ambayo yanawajibika kwetu kwa hesabu zake na pia ufanisi wake kwa ujumla. Tumefanya hivyo pia katika mashirika mengine, hili la TANESCO sio tukio la kipekee;
  3. Kitendo hiki cha halali na kwa mujibu wa Kanuni kilichofanywa na Kamati yangu kimetafsiriwa kwa makusudi na baadhi ya watu kwamba ni ishara ya kuwa sisi au zaidi kwamba mimi nina maslahi binafsi na TANESCO na hususan Mkurugenzi wake Injinia Mhando, ndio maana tumetaka maelezo ya Bodi. Ukweli kwamba Kamati ya POAC tumewaita pia Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu (CAG) na Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) kwa jambo hilo hilo umefichwa kwa makusudi!
  4. Baada ya tukio hilo, nikiwa hapa Dodoma, mwandishi wa habari wa gazeti moja alinifuata akiniambia kuwa wamekutana na Mhe. Waziri Mhongo na Katibu Mkuu wake, Nd. Eliachim Maswi hapa hapa Bungeni na wamewaambia kuwa mimi nimepewa rushwa. Hakutaja nimepewa rushwa na nani, kiasi gani na wala kwa lengo gani!
  5. Nimejaribu kumtafuta kwa simu Mhe. Waziri Mhongo na Katibu Mkuu wake ili wanipe ufafanuzi juu ya mimi na Kamati ya POAC kuhusishwa na tuhuma hizi bila mafanikio, hali ambayo inaniondolea mashaka juu ya ushiriki wao katika kueneza au kuthibitisha uvumi huo. Najaribu sana kujizuia kutokuwa na mashaka na ushiriki wao huo ikizingatiwa uzito na taswira ya nafasi zao katika jamii, lakini wameshindwa kunidhihirishia tofauti.
Sasa naomba kutoa ufafanuzi rasmi kuhusu mlolongo wa matukio hayo tajwa ambayo yanatumiwa na baadhi ya wanasiasa kuonesha kwamba eti nimehusika na vitendo vya rushwa.
  • Binafsi sijawahi kuwa na mawasiliano ya aina yeyote na uongozi wa TANESCO kushawishiwa juu ya hatua ambazo POAC ndio imezichukua za kutaka kujiridhisha juu ya utaratibu uliotumika. Ieleweke wazi kabisa kuwa, hakuna wakati wowote, popote ambapo mimi binafsi au Kamati yetu imekataa Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO kuchunguzwa kwa tuhuma zozote. Ambacho tumesisitiza wakati wote ni ufuatwaji wa taratibu, kanuni na sheria, hili nitalisimamia iwe masika au kiangazi;
  • Ni kwa sababu hiyo, na kwa kujiamini kabisa nimeunga mkono suala la tuhuma za rushwa zinazotajwa zichunguzwe na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kwa kina;
  • Nimekwenda mbali zaidi kukiomba chama changu CHADEMA kifanye pia uchunguzi na tathmini yake kwa kina kujiridhisha na tuhuma hizo;
  • Natumia fursa hii pia kuomba vyombo vya Dola vichunguze tuhuma hizo kwa nafasi yake ili kuweza kupata ukweli;
  • Ninaahidi kushiriki kikamilifu iwapo nitatakiwa katika uchunguzi wowote utakaofanywa na niko tayari kuwajibika iwapo nitakutwa na hatia yeyote.
Napenda niwatoe hofu wananchi wa jimbo la Kigoma Kaskazini walionituma kuja kuwawakilisha hapa Bungeni na Watanzania wote kwa ujumla kwamba:-
  1. Mimi Zitto Zuberi Kabwe sina bei, sijawahi kuwa nayo na sitarajii kuwa nayo huko mbeleni. Daima nimesimamia kidete maadili ya uongozi bora katika maisha yangu yote ya siasa, na nawaahidi sitarudi nyuma katika mapambano dhidi ya rushwa katika nchi hii pamoja na mikakati ya aina hii ya kunidhoofisha na kunivunja moyo;
  2. Nafarijika na salam mbali mbali zinazotolewa kunifariji na kusisitiza kuwa nisilegeze kamba katika mapambano haya, nimepokea ujumbe mwingi kwa simu, sms, tweeter na hata facebook na niko pamoja nanyi Watanzania wenzangu kamwe sitarudi nyuma hadi kieleweke. Naamini katika nchi yetu tunazo rasilimali za kutosha mahitaji/haja ya kila mmoja wetu lakini si ‘tamaa/ulafi’ wa baadhi ya watanzania wenzetu;
  3. Napenda kuweka rekodi sawa kwa Watanzania kwamba nimekuwa Mbunge hiki ni kipindi cha pili, Mimi ni Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) huu ni takriban mwaka wa saba sasa, Kamati yangu inasimamia mashirika 259 ya Umma na si TANESCO peke yake. Mchango wa Kamati hii katika Bunge na kwa ustawi wa Mashirika ya Umma ni bayana na haujawahi kutiliwa shaka. Kamati yetu imeokoa upotevu mkubwa wa mali za umma na kuokoa fedha za umma kutokana na umakini wake. Tumefanya hivyo CHC hivi karibuni, Kiwira na kwenye mashirika mengine mengi. Kote huko uadilifu na uzalendo wa Kamati hii haujawahi kuhojiwa. Inatuwia vigumu kuona kuwa tunahojiwa katika suala hili la TANESCO. Hapa pana kitendawili.
  4. Zipo hoja pandikizi za kutaka Kamati ya POAC ivunjwe na haswa zikinilenga mimi binafsi. Nafahamu kiu ya wasioitakia mema nchi yetu kuiona POAC ikivunjwa au sura zikibadilishwa kwa kuwa Kamati hii imekuwa mwiba kwa mikakati yao ya kifisadi. Kwa maoni yangu, Kamati ya POAC isihusishwe na tuhuma hizi kwa vyovyote vile. Niko tayari nihukumiwe mimi kama mimi na sio kuhusisha wajumbe wengine ambao hawatajwi mahala popote katika tuhuma hizi mbaya sana katika historia ya Bunge letu. Nitakuwa tayari kunusuru Kamati ya POAC na maslahi ya taifa letu kwa kujiuzulu Uenyekiti iwapo itathibitika pasipo shaka kuwa nimehongwa. Kamati ya POAC ni muhimu zaidi kuliko mimi.
  5. Nafahamu pia kuwa kuna wanasiasa hasa wa Upinzani ambao wanautaka sana Uenyekiti wa POAC na wanafanya kila njia kutaka kuidhoofisha. Lakini hawajui kuwa anaepanga wajumbe wa Kamati ni Spika wa Bunge.
  6. Msishangae pia kuja baadae kubaini kwamba baadhi ya wanasiasa wenye midomo mikubwa ya kutuhumu wenzao wao ndio vinara wa kupokea rushwa.
  7. Ni lazima tufike mahali kama viongozi kwamba utaratibu unapokiukwa na yeyote yule, au uongo unapotolewa hadharani tuseme bila kuogopa. Hili ndio jukumu letu kama wabunge na viongozi. Kusimamia ufuatiliaji wa utaratibu ni jukumu letu kama Kamati ya POAC na ndio sababu ya msingi ya kuanzishwa kwa mamlaka kama CAG na PPRA. Haiwezekani, tuwe na set ya kanuni kwa kundi fulani na nyingine kwa makundi mengine, au kuhukumu ufuataji wa taratibu kwa kuangalia sura ya mtu usoni.
Mwisho
Kumejengeka tabia hivi sasa ya kuwamaliza wanasiasa wenye kudai uwajibikaji na uzalendo. Kumeanzishwa kiwanda kwenye medani ya siasa cha kuzalisha majungu na fitna zenye lengo la kuwachonganisha wanasiasa wa aina hiyo na wananchi kwa kutumia vyombo vya habari na nguvu ya fedha. Naamini mbinu hizi chafu, kama nyingine nyingi zilizojaribiwa kwangu huko nyuma nazo zitashindwa.
Naamini katika kweli na kweli daima huniweka huru. Naamini kuwa mwale mdogo wa mwanga wa mshumaa hufukuza kiza. Kwa imani hiyo, sitasalimu amri mbele ya dhamira zao ovu hata nitakapobaki peke yangu katika mapambano hayo ya kulinda na kutetea rasilimali za taifa zinufaishe watanzania wote.
Daima nitaongozwa na busara ya Hayati Shabaan Robert isemayo, ‘Msema kweli huchukiwa na marafiki zake, nitakapofikwa na ajali hiyo, sitaona wivu juu ya wale wawezao kudumu na marafiki zao siku zote, siwezi kuikana kweli kwa kuchelea upweke wa kitambo, nikajitenga na furaha ya kweli itakayotokea pale uwongo utakapojitenga”.
Ahsanteni sana.

SOURCE: MEDIA2SOLUTION

Rais wa Zanzibar Dk Ali Shein Katika Ziara Maalum Ya Mikoa Ya Kusini na Kaskazini Pembe

Tweeted this Like this, be the first of your Friends
  Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein,akisalimiana Kaimu Mwenyekiti wa Tume ya Katiba Dk Salim Ahmed Salim na Viongozi mbali mbali,wa Chama na Serikali, alipowasili katika uwanja wa Ndege wa Karume Pemba jana akiwa katika ziara maalum ya Mikoa ya Kusini na Kaskazini.
  Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein,na Mkewe Mama Mwanamwema Shein,wakisalimiana na Viongozi mbali mbali,wa Chama na Serikali, alipowasili katika uwanja wa Ndege wa Karume Pemba jana akiwa katika ziara maalum ya Mikoa ya Kusini na Kaskazini.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Ali Mohamed Shein,akisalimiana na Viongozi wakuu wa Vikosi vya Ulinzi Pemba, alipowasili katika uwanja wa Ndege wa Karume Pemba jana akiwa katika ziara maalum ya mikoa ya Kusini na Kaskazini.Picha na Ramadhan Othman,Ikulu-Zanzibar

TAMKO LA CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)KUHUSU KUFUNGIWA KWA GAZETI LA MWANAHALISI

Tweeted this Like this, be the first of your Friends

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kinalaani uamuzi wa Serikali inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kulifungia kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi kwa kutumia mwanya wa sheria mbovu ya magazeti inayokwenda kinyume na haki za binadamu na utawala bora.

CHADEMA kinaitaka Serikali kulifungulia gazeti hilo haraka iwekanavyo na kimewasiliana na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inayoongozwa na CHADEMA kuchukua hatua za kibunge kuisimamia Serikali  kurekebisha udhaifu huo ikiwa inaheshimu uhuru wa habari na inazingatia maslahi ya taifa.

CHADEMA kinatafsiri hatua hiyo ya Serikali ya kufungia gazeti la MwanaHalisi kuwa ni sawa na kufungia uhuru wa kusambaza habari, uhuru wa kupokea habari na uhuru wa kutoa maoni, hivyo tunatoa mwito kwa wananchi na wadau wote wa habari kuungana pamoja kupinga hatua hiyo, na CHADEMA kitaeleza hatua za ziada za kuchukuliwa iwapo Serikali haitasikiliza kauli za wadau wa habari juu ya suala hili.

CHADEMA kinatambua kuwa uamuzi wa Serikali kufungia gazeti hilo kwa mara nyingine tena ni kwenda kinyume na haki za binadamu, kinyume na utawala bora na ni kikwazo kwa demokrasia na maendeleo nchini.

CHADEMA kinapinga hatua ya Serikali ambayo viongozi na watendaji wake wakiwa wametajwa kama watuhumiwa katika habari zilizoandikwa na gazeti hilo imetumia mamlaka haramu ya Waziri mwenye dhamana ya sekta ya habari kugeuka mlalamikaji, mwendesha mashtaka na mfungaji huku ikipuuza taasisi za kusimamia uwajibikaji na haki.

CHADEMA ilitarajia badala ya kulifungia gazeti la MwanaHalisi ingewezesha kufanyika kwa uchunguzi huru kufuatia habari za kiuchunguzi zilizoandikwa na gazeti hilo juu ya watendaji na watumishi wa Serikali kuhusishwa na jaribio la mauji ya Dr Ulimboka Steven, kupanga njama za mauji ya viongozi wa CHADEMA na matukio mengine ambayo yenyewe ndiyo yenye mwelekeo wa kufanya wananchi wapoteze imani na vyombo vya dola hali ambayo inaweza kuhatarisha amani na mshikamano uliopo nchini.

CHADEMA kinalinganisha uamuzi huo wa Serikali uliotangazwa tarehe 30 Julai 2012 na Msajili wa Magazeti chini ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo  kuwa ni sawa  kujichukulia sheria mikononi kwa kuwa Serikali yenye kuheshimu misingi ya asili ya haki ingezingatia kwamba ikiwa chombo chochote cha habari kimedaiwa kuvunja sheria ama kukiuka maadili dhidi ya Serikali, viongozi wake ama watu binafsi mashtaka au malalamiko yangepelekwa kwa taasisi zinazohusika mathalani Baraza la Habari (MCT) au mahakama.

CHADEMA kinafahamu kuwa Serikali imeamua kulifungia kutochapishwa kwa muda usiojulikana gazeti la MwanaHalisi, kwa mujibu wa Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, kifungu Na. (25) (i); hata hivyo uamuzi huo ni kinyume cha misingi ya asili ya utawala wa sheria.

CHADEMA kinaelewa kwamba zipo sheria nyingine katika nchi yetu ambazo Serikali ingeweza kuzitumia kushughulikia madai iliyoyatoa kuwa Gazeti la Mwanahalisi limeandika habari na makala za uchochezi, uhasama na uzushi kupitia mahakama lakini imeamua kwa makusudi kuendelea kutumia sheria mbaya isiyokuwa na uhalali wa kihaki (illegitimate).

CHADEMA kinakumbusha kuwa kwamba Sheria hiyo ni kati ya Sheria zilizotajwa na Tume ya kukusanya maoni juu ya mfumo wa vyama vingi (Tume ya Nyalali) kuwa ni sheria mbaya miaka 20 iliyopita kuwa na Sheria mbaya na Serikali imekuwa ikikwepa kutunga sheria mpya pamoja na wadau wa habari kuandaa miswada ya sheria ya huduma za vyombo vya habari na uhuru wa taarifa kwa nyakati mbalimbali.

CHADEMA kinatoa mwito kwa wananchi na taasisi zote za kitaifa na kimataifa kufuatilia kwa karibu tukio hili la kufungiwa kwa gazeti la MwanaHalisi na matukio mengine ya hivi karibuni kuhusu asasi za kiraia, makundi mbalimbali katika jamii ikiwemo madaktari na vyama vya siasa hususan CHADEMA yenye kuashiria kwamba Serikali inayoongozwa na CCM imeanza mkakati wa kuficha ukweli na kudhibiti mabadiliko kwa kutumia sheria kandamizi, vyombo vya dola na njia nyingine haramu.

Hivyo, ieleweke kwamba hatua hii dhidi ya Gazeti la MwanaHalisi ni mwanzo tu wa hatua zingine zaidi dhidi ya magazeti mengine na taasisi nyingine hali ambayo inahitaji wananchi na wadau wote kuunganisha nguvu za pamoja katika kuchukua hatua za haraka kuinusuru nchi na mwelekeo huo.

Imetolewa tarehe 30 Julai 2012 na:

John Mnyika (Mb)
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...
 
Web Directories
PageHeat